Picture Gallery Send us feedback

NEWS

Hip hop yaenguliwa tuzo za Kili!

Muziki wa hip-pop umeondolewa katika mashindano ya mwaka huu ya tuzo ya mwanamuziki bora, Kili Music Awards, yatakayoanza mwishoni mwa mwezi huu katika ngazi za kanda na fainali kufanyika Mei.

Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, ambao ndio wadhamini wa mashindano hayo, Oscar Shelukindo alisema jijini juzi wakati wa uzinduzi wa mashindano kuwa muziki huo umeondolewa kutokana na kuwa vigumu kupata albamu iliyokamilika.

Hata hivyo, Shelukindo alisema pamoja kwa kuondolewa muziki huo, mashindano ya mwaka huu yatashirikisha aina 24 za muziki, ambazo zipo zilizoongezwa kutokana na kuonekana kuwa na ushindani.

``Mambo mengi ya mchanganuo wa mashindano tutatoa baadaye wiki ijayo ila tu mwaka huu tutakuwa na categories nyingi tofauti na mwaka jana,? alisema Shelukindo.

Alisema mwaka huu kutakuwa na kanda nne ambazo ni Kaskazini, Kusini, Ziwa na Kati, ambazo washiriki wake watapambana na kupatikana kwa mshindi mmoja atakayekuja ngazi ya taifa kwa kila aina ya muziki.

Alisema kampuni ya bia nchini, TBL, itaendelea kudhamini mashindano hayo kwa kipindi cha miaka mitano ijayo kuanzia mwakani, baada ya kumaliza kipindi kama hicho mwaka huu.

``Kampuni inatumia zaidi ya milioni 200 kwa mwaka kwa ajili ya mashindano haya, hivyo tumeongeza miaka mingine mitano kwa ajili ya kuendesha mashindano haya, ambayo yanatoa fursa kwa wasanii wa Tanzania kuonyesha vipaji vyao,`` alisema.

Pia alisema tuzo hizo zitaboreshwa ili ziweze kutambuliwa kwa Afrika Mashariki na Kati, kwa msanii aliyepata kuweza kupambanishwa kutokana na sifa na ubora wake, pia washindi wataendelezwa kwa kupata programu za maendeleo ambapo watashirikiana na Baraza la Sanaa la Taifa, (BASATA).

Naye mwakilishi kutoka BASATA, Anjelo Luhala alisema TBL kupitia tuzo hiyo inaendeleza sera ya utamaduni ya mwaka 1997, ambapo tayari wamewawezesha wanamuziki 120 kupata tuzo hizo kutokana na kazi zao.

Luhala alisema sasa muziki wa Tanzania umekua na kujulikana nchi mbalimbali na kufanya kazi za wasanii kupata soko kubwa.

``Tunachukua fursa hii kuwapongeza TBL kwa kuwawezesha wasanii wa Tanzania muziki wao kuwa na soko ambalo linaongeza kipato chao, `` alisema Luhala.

Hata hivyo, aliwataka wasanii hao kubadilika kwa kujiendeleza katika taaluma ya muziki, pia wawe wajasiriamali kwa kujijengea mitaji na kuanzisha vikundi vya Saccos na wajue haki zao zinazolinda maslahi ya kazi zao, kuepuka kulanguliwa na watu wasiopenda maendeleo yao, kwani ulimwengu wa sasa hauendi kwa kubahatisha.

Mpigie kura msanii au bandi uipendayo PIGA KURA SASA!!!!!

 
Habari zaidi