HABARI/NEWS

Mtanzania ang'ara Marathon India

MWANARIADHA aliyeanza kujinyakulia umaarufu katika mbio za nyika nchini, Osward Reveline wa mjini hapa, ametwaa medali ya fedha katika mashindano ya kimataifa ya marathon nchini India.

Mwanariadha huyo ambaye ni mtumishi wa Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro, alitwaa medali hiyo baada ya kushika nafasi ya pili kwenye mashindano hayo yaitwayo Pune yaliyofanyika mwishoni mwa mwezi uliopita.
Matokeo ya mashindano hayo yaliyotolewa na Pune International Marathon yameonesha mwanariadha huyo alitumia muda wa saa 02:19:23, ambapo aliyeongoza ni wa Swedeni, Said Regragoui, aliyetumia muda wa 02:18:23.

Matokeo hayo ambayo Majira inayo nakala yake yamewataja walioingia kwenye kumi bora kuwa ni Josephat Ndeti, Elkanah Machuka, Ambrose Makau, Lezan Kimutai wote wa Kenya.

Katika mashindano hayo ambayo nchi zaidi ya kumi zilishiriki, wengine kwenye kumi bora ni Abebe Siyoum, Gemechu Kabede na Girma Fente wote kutoka Ethiopia na Ruslan Deulin wa Russia.

Hata hivyo, aliyewahi kuiletea Tanzania medali ya dhahabu katika mashindano ya Marathon ya Jumuiya ya Madola nchini Uingereza, Francis Naali alishika nafasi ya 12.

Katika mashindano hayo yaliyomalizikia Uwanja wa Nehru, baada ya kuanzia Kandoji Baba Chowk na kuuvuka mara mbili mto Mutha kabla ya kumalizikia uwanjani hapo, msichana wa Tanzania, Monica Samira alikuwa wa 12 pia.

Kwa upande wa wasichana katika mbio za nusu marathon kwenye mashindano hayo ya Pune, ambayo Wakenya walitamba katika nafasi tatu za juu, ni Hellen Musyoka aliyetumia saa 01:13:20 na kushika nafasi ya kwanza.

Pia Mkenya, Cathy Mutwa alikuwa wa pili na Pauline Mutwa alikuwa wa tatu, ambapo wengine kumi bora ni Helaria Johanes wa Namibia, Jane Muia wa Kenya, Serkalem Bisset na Gtenesh Urge wa Ethiopia, Madhuri Gurnule na Preeti Rao wa India na Gittee Karlshoj wa Denmaki.